NDOA inapovunjika kuna kuna mambo
makuu matatu ambayo hutokea kutokana na ndoa hiyo kuvunjika. Kwanza ni kugawana
mali walizochuma wanandoa, pili hifadhi ya watoto na tatu matunzo ya watoto.
Haya ni matokeo ya kuvunjika kwa ndoa, mengine zaidi kuhusu kuvunjika kwa ndoa
tutayaona hapa wakati nikieleza mgawanyo wa mali za wanandoa.
1.MALI ZIPI
HUTAKIWA HUGAWANYWA NDOA INAPOVUNJIKA? Ndoa inapotangazwa kuvunjika, mali
ambazo hupaswa kugawanywa ni mali za wanandoa wenyewe. Swali mbele yetu ni kuwa
ni zipi mali za wanandoa? Mali za wanandoa ni zile zote zilizochumwa na
wanandoa hao kwa jitihada au juhudi za pamoja wakati wa ndoa yao. Mali hizo
zaweza kuwa zinahamishika au hazihamishiki. Mali zisizohamishika ni kama
nyumba, viwanja, mashamba n.k. Mali zinazohamishika ni kama magari, baiskeli,
pikipiki,vifaa vya ndani kama fenicha, fedha benki, na mali nyingine ambazo
hazionekani kwa macho au hazigusiki kama hisa n.k. Zingatia sana usije
kudhulumiwa kwa kuwa hata hisa pamoja na akiba ya fedha benki nayo ni mali
inayostahili kugawanywa.























